Super Bets Dar Kikaangoni Kwa Kushindwa Kumlipa Mteja Aliyeshinda Milioni 160


Mkeka umegeuka shubiri kwa kampuni ya michezo ya bahati nasibu na kubashiri matokeo ya michezo, Super Bets ya jijini Dar es Salaam baada ya kushindwa kuwalipa wateja wake waliodai kushinda kiasi kikubwa cha fedha.

Mmoja kati ya wateja hao anadaiwa kushinda shilingi milioni 164 Jumatatu hii. Msimamizi wa Super Bets aliyejitambulisha kwa jina la Amani, aliongea na kipindi cha Sports Extra cha Clouds FM kuwa watu hao walishinda kimakosa. Amedai kuwa moja ya vyanzo vinavyowapatia matokeo ambayo kwenye mkeka zinaitwa odds ilikuja ndivyo sivyo.

“Baada ya hapo timu yetu ya masoko ilipogundua kuna tatizo hilo limetokea ina maana wakaja wakalifanyia kazi wakatujulisha tukagundua kuwa kuna tatizo fulani lilitokea tukalifanyia marekebisho. Baadhi ya wateja walikuja hapa wakasema wameshinda kutokana na zile odds za 98, tukawaambia wasubiri kwamba tunalishughulikia kwamba kuna matatizo ya kimtandao yalitokea. Tutawalipa kutokana na correct odds ambazo zilitolewa katika mtandao baada ya kurekebishwa hilo tatizo,” alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa bodi ya michezo ya kubahatisha nchini, Abbas Tarimba amedai kuwa wateja hao wamewasilisha malalamiko yao na wanayafanyia kazi.

Amedai kuwa maafisa wa bodi hiyo walienda kwenye ofisi za Super Bets kufanya uchunguzi kwenye server zao ili kubaini ukweli na wamewaomba walalamika siku mbili kukamilisha uchunguzi huo.

Miaka ya hivi karibuni betting kwenye michezo imekuwa biashara kubwa huku kukiwepo na makampuni mengi yanayochezesha na kuwavutia watu wengi hasa vijana.
Previous
Next Post »

Total Pageviews